Thursday, April 28, 2011

HIZI NI KUMBUKUMBU ZA ALI SHETANI AMBAYE ALIKUWA NI KOMRED AU(( UMMA PART))

Ramadhan MadafuI am not worried about “kibuki” because I may be an even more powerful shetani. In the streets, people sometimes even call me “Ali Shetani” as a joke.                        Ali Sultan Issa
Jina la Ali Shetani sikuanza mimi hapa. Hili ni jina analojisifu mwenyewe katika kumbukumbu zake alizo andika kwenye kitabu chake kilicho toka hivi karibuni. “Race, Revolution and Struggle for Human Rights in Zanzibar – The Memoirs of Ali Sultan Issa and Seif Sharif Hamad” (page 162).
Hapa nitakipitia kitabu hichi muhimu katika historia ya visiwa vyetu vipenzi vya Unguja na Pemba. Humu katika kitabu hichi tunapata kuwajua makomred, wafuasi wa Umma Party iliyo ongozwa na Ali Sultan pamoja na Babu. Humu tunaupata ukweli wao kwa ulimi wa kiongozi wao mkubwa kabisa. Sio kwa kuzuliwa na Mahizbu, Ma-ZPP, Ma-afro au Ma-youth-league. Humu tunapata kujua tabia za makomred kwa wanavo taka wenyewe tujuwe.
Ali Shetani ndie kiongozi hasa wa makomred.
Babu ni wapili katika chama hichi. Ali anatueleza  kwamba alipofika London, Ungereza August 1953, hakuchukua muda kuingia chama cha kikoministi, May Day 1954 (Page 50). Wakati huo Babu akijiona yeye ni anarchist, (page 49). Ali Shetani anatuambia kua yeye ni Mzanzibari wa kwanza kwenda Moscow 1957, (page 54).
Shetani kafukuzwa  kutoka ZNP kwa sababu ya kuponda viongozi wa chama chake. Anatueleza kwamba alipokua Babu yuko jela, Ali Sultan ameanzisha mpango wa kuunda chama cha tatu. Alizungumza na vijana, wafanyakazi, makomred wenziwe ndani ya ZNP na baadhi ya viongozi wa ASP walio soma Urusi kama Moyo, Twala, na Hanga.  Anatuambia kwamba: “sikuwa na niya ya kufanya lolote bila ya Babu kukubali, lakini tulitaka akitoka jela akute mambo yote yamekwisha bila yakuweza kuyahoji au kuyageuza (fait accompli)” (page 77).
Alipotoka Babu jela, Shetani anatuambia: “hapo hapo nilimtilia nguvu Babu atoke ZNP”. Babu akasema: ”Wacha kwanza tujenge umoja na masikilizano na tukurejeshe kwenye chama”. Anaendelea Komred Ali Sultan kusema: “Babu alitaka kusikilizana mpaka siku ya mwisho”.
Nani Ali Sultan Issa?Kwa vipimo vyetu vya visiwani na kwa murwa wetu wa Kiislamu au hata wa Kibinadamu huyu kiongozi wa makomred simtu wa maana. Bora tumuachie mwenywe atueleze.
Mama yake malaya: Tumsikilize Ali Sultan kuhusu mama yake mzazi: “Sijui vipi mama yangu akiweza kutulisha. Inaweza kuwa akipata pesa kwa wanaume wake.”, ( page 37). Naam huyu ni mama yake mzazi. Anamsifu kuwa alikuwa ana wanaume wake ambao wakimlipa pesa huyo mama kwa huduma zake.
Mlevi: Komred Shetani anatuelezea kuwa alipokuwa chini wa umri wa miaka 13 mama yake akimchukua huyu mtoto kwa mjomba wake na akimpa vinibu vya brandy au wisky na chochote kile kiliopo. Baadae alipotimia miaka 13 akaanza kulewa mwenyewe kwa kunya tembo la mnazi, (page 39). Ameendelea na ulevi mpaka hii leo.
Anakula nguruwe: Anasema Komred: “Nilipokua Cuba mara ya pili, nilialikwa kwenye karamu ya rasmi, ghafla akafika Fidel Castro. Nilikua nimeshika sahani ya mhogo na nguruwe, yeye (Castro) akaja, akacheka na mie, akaniambia ‘Yukko con poyo’, maana yake mhogo na nguruwe.”, (page 77).
Hamhishimu baba yake: Baba yake Ali Sultan alikataa kumposea mke. Anaelezea kuhusu mkewe wa mwanzo: “Baba yake (Amour  Zahor) na mimi tulikua sote memba wa halmashauri kuu ya ZNP. Yeye alikua Unguja na mimi nilikua Pemba. Nimesikia baadae hakunikubali kuoa mwanawe kwajili mie siamini dini.”, (page 57). Anaendelea: “Baadae viongozi wa chama wamekuja kutupatanisha mie na baba yangu. Wamesema nae kwanza na baadae wakanijia mie. Wamenitaka nimuangukie miguu na nimtake radhi. Nikakataa, nikawaambia yeye ndie mkosa, kwa hivyo yeye (baba yangu) ndiye aniangukie miguu na anitake radhi”, (page 58).
Anachukua wake za watu: Anaelezea alipo mchukua mke wa mwenziwe alie fungwa baada ya mapinduzi, akamkodia nyumba: “Niliita nyumba yake “makimbilio” kwani huko ni pahali ninakokwenda jificha. Ni pahali pakuzini”. Alipotoka mumewe jela Shetani alimuambia: “Nilikuwekea mkeo ulipo kua hupo, sasa huyu hapa. Ninakurejeshea mwenyewe”, (page 102). “Pia nilikuwa nina nyumba yangu maksudi ya kuzinia”, (page 120)
Mvuta bangi: Ali Shetani kaanza kuvuta bangi tokea mtoto wa miaka13. Anaelezea: “Nilipokua waziri, kuvuta bangi asubuhi kukinipa nguvu na uwezo wa kufikiri. Nikitaka kuandika kitu, ninavuta bangi, hapo fikra zinakuja”, (page 118)
Jasusi: Alipokuwa katika ZNP alipelekwa Misri kufungua ofisi ya ZNP Cairo. Huko Cairo alitengeneza maandamano alipo uliwa Petrice Lumumba. Wakaingia ubalozi ya Belgiji. Huko Waliiba makaratasi ya siri ya ubalozi, akawapa makaratasi hayo Marusi, Machina na Machekoslovakia. Ama Wamisri walipewa matakataka tu. (page 67-68).
Baada ya mapinduzi, Abeid Karume alijuwa uhodari wake Komred Shetani wa ujasusi, akampleka ubalozi wa Zanzibar London kufanya kazi chini ya Othman Shariff. Kazi yake huko ilikua “kumchungua (Othman) kila anachofanya”, (page 97). Tunajua Nyerere na Karume wameshirikiana kumuuwa Othman Shariff, (page 129), na Komred Ali ndie alie ripoti kila alichokuwa akifanya huko London. Pia tunajua Nyerere na Karume wameshirikiana kumuuwa Hanga na Twala (page 130-131), na makomred walimuandama Hanga na Twala kwa muda mrefu kabla ya mapinduzi (page 77).  Je! makomred wameshirikiana vipi kuwadhulumu vijana hawa? Tunangojea makomred wengine waungame.
Na mengineo: Anatuelezea mwenyewe Komred Ali alipo onana na Frank Carlucci huko pemba. Carlucci alikuweko Kongo alipo uliwa Lumuba, baadae akaletwa na CIA Zanzibar siku za mapinduzi. Mwisho akawa mshauri wa Rais Regan kwa mambo ya usalama kisha akawa waziri wa ulinzi, Marekani. Baada ya mazungumzo marefu baina ya Shetani na mjumbe wa CIA anasema Shetani: “Mpaka hapo tumekwisha imaliza liter kasrobo ya Wisky tokakubaliana tukhitalifiane. Kwa bahati nzuri, mke wangu alkwenda mbali kuhudhria mkutano, kwa hivyo nikamuambia (Carlucci) tulale pamoja kitandani.” (page 96).
Ali Shetani kaanza Pemba“Nimekaa Pemba chini ya miezi miwili, na sikumbuki kufanya jambo lolote la kujuta hii leo. Nitafanya yale yale kwa njia ile ile hii leo.”,      Ali Sultan Issa (page 93).
Abeid Karume alimpeleka Shetani Pemba baada ya mauwaji ya Unguja. Anaelezea Komred Ali Sultan kwamba Wahindi na Warabu waliotaka kuhama Pemba kukimbilia Kenya au Tanganyika ilibidi wanyakanywe dhahabu zao. “Hatukutaka kitu chochote kengine, dhahabu na mapambo (jewelry) tu.”, (page 90)
Akaanza Komred Shetani kupiga watu viboko. Anaeleza: “Badala yakutia watu jela, kila mkosa akipigwa viboko halafu anaachiliwa…. Niliona hivi ni bora kuliko kuwatia jela……Basi nikikaa kitini markiti, nikawa nagawa adhabu. Tukiwapiga watu viboko hadharani, ili watu wote waone, ili washike adabu zao.”, (page91)
“Sikupenda kulazimisha watu kazi, lakini kazi kwa hiari pamoja na kuwapa moyo”. “Baadhi ya wakati ninachukua fimbo njiani ninafukuza yoyote asiefanya kazi, na asiejenga nchi”. “Kwanza ninazungumza nao na ninajaribu kwahamasisha kwa maneno. Lakin baadae sisiti kuwapiga watu viboko nikiwaona wamekaa wakati wa kazi.”, (page 95)
Makomred na Mali ya WatuAli Sultan alikua mkubwa wa halmashauri ya kutaifisha majumba. anajisifu kunyang’anya majumba ya watu wa Mjini Unguja. “Katika miezi minne na nusu niliotumikia halmashauri hii tumenyang’anya majumba mamiya. Aghlabu ya nyumba za mawe Mjini tumezinyang’anya”, (page 101). “Kwa kuondoka Warabu na Wahindi walibakia Mjini watu wachache sana ambao wakiishi huko kabla ya mapinduzi, labda kumi katika asili miya..  Walivo ondoka wote hao, majumba mengi Mjini yakawa matupu na yanaporomoka. Mjini kukawa kama msitu, yoyote anaweza kujificha akitaka.” (page 125).
Baada ya kunyang’anya watu majumba, mashamba, mali na maduka yao nini wamefanya makomred? Shetani hakuacha kutuelezea: “Tulipo maliza kujenga nyumba yetu nzuri Migombani baharini, kusini ya mji wa Zanzibar. Maria (mkewe wa pili) na mie tumeipanga wenyewe nyumba yenye veranda na mandhari nzuri ya bahari. Ina njia ya miguu kuteremkia mpaka mchanga wa pwani. Tulikuwa na vyumba saba, vyoo viwili na garaji. Kulikuwako majiko mawili, moja ndani ya nyumba na moja nje. Kulikuweko upande wa maboy na choo chao. Sakafu ya nyumba ilikuwa ya saruji, kwa hivyo tukiwa na sherehe tunawakiribisha wageni huko. Juu tulikua na chumba changu cha kusomea, pahala pa kuweka mabuku, kijiko kidogo, na bar. …..Nje barabarani nimeweka bao kuwaambia kila apitae ‘Azimio la Mapinduzi’, kwani nilihisi kujenga nyumba kama hii ndio makusudio ya mapinduzi.” (page 121)
Ali Sultan alichukua eka tatu meli nane kaskazi ya Mjini, na eka tisa Machui, (page 128). Baadae kachukua eka 27 Chuini kajengea hoteli yake (page 154).
Maisha ya Kikomred
“ Tulikuwa wana wa mapinduzi na nilazima tujitolee mhanga baadhi ya raha zetu”,
Ali Sultan Issa (page 118).
Ali Shetani, mkubwa wa makomred na koministi wa kwanza Zanzibar anatueleza vipi maisha yake: “Natumia kiasi dola 60 kwa sigara na Dola 180 kila mwezi kwa ulevi. Pia ninawaajiri maboy wawili na mayaya wawili kunichungia kibanda changu Chuini  au kupika na kusafisha nyumba. Kwa pamoja, wote wanne wanapata Dola 75.” (page 163). Huyu ndie Komred mkubwa, mpiganiyaji wa haki za wafanya kazi na wakulima na wanyonge. Anatumia pesa zaidi ya mara tatu kwa sigara zake na ulevi wake kuliko mishahara wa watu wanne wanao mtumikia.
“Nilpokuwa waziri, maisha yangu binafsi yalikuwa bora sana kuliko watu wa dasturi. Mshahara wa kuanzia mwalimu wa serekali ulikua shilingi mia tatu kwa mwezi. Mimi nikipokea shilingi elfu tatu……pamoja na gari, dereva, petroli, kodi ya nyumba, maji, taa na telefoni bure.” (page 119).
“Karibu ya nyumbani  ulikuweko mti wa Mabanyani mkubwa, mpaka leo upo. Mtoto wa Kiarabu  wa kiasi miaka kumi akiuparamia mti mpaka chini ya dirisha la chumba cha wanangu. Akikaa kwenye mti akiwachokoza na kufanya mzaha na wanangu, mpaka siku moja nimechoka nae nikaamrisha polisi wamkamate  na wamtupe jela. Kwa hakika polisi wamechukua hatua mahususi kwa sibabu nilikua waziri. Baada ya kiasi wiki moja, mama yake kanijia akaniomba nimtoe jela. Nikamtoa. Siku zile sisi mawaziri tukiweza kumkamata na kumfunga yoyote tunaye mtaka…tulikuwa na nguvu hata ya kuuwa.”, (page 120-121)
Hata mwanaharamu wake akimuogopa na akimkibia: “Alikua ni mwanangu mwanamume wa kwanza. Ninapo kwenda kwao, mwanzo akinikimbia kwa sibabu nilikua waziri na kila mtu akiniogopa.” (page 122)
Makomred na ilimu
“The standard of education went down, and the single person most responsible for this deterioration was Ali Sultan Issa.”            Seif Sharif Hamad (page 195)
Ali Sultan kiongozi wa makomred alikamata kwa muda wa miaka minne wizara ya ilimu ya Zanzibar baada ya mapinduzi. Bora tumuachilie mwenyewe atuelezee aliyo yafanya.
Kata mishahara ya walimu: Komred Ali Shetani amekata mishahara ya walimu kutoka shilingi mia sita mpaka mia tatu. Anasema: “Baada ya kupunguza mishahara, mwalimu Zanzibar akipata mshahara sawa sawa na askari wa polisi au mwanajeshi.” (page 110).
Fukuza walimu: “Wale walimu wasiokubaliana na siasa yetu wemetokelea mbali. Wale waliobaki hawakusema chochote kwa sibabu wakiogopa” (page 110)
Mafunzo ya Kiislamu: Shetani anasema: “Mafunzo ya Kiislamu Zanzibar yameanguka chini baada ya mapinduzi, kwa sababu mashekhe wengi wameacha nchi. Sisi makomred tumeona hili ni jambo zuri. Visiwa vyote hivi vilikua Waislamu. Wanataka nini tena? Badili ya mashekhe kuja huku, nawende kwengineko kwenye watu wanaotaka kusilimishwa.” (page111)
Ushahidi wa Seif Sharif: Seif Sharif kamaliza masomo yake ya form six Unguja Novemba, 1963. Januari 1964 nchi imepinduliwa. Kufika March 1964 Seif kawa Maalim Seif. Baada ya miezi minne kumaliza skuli, amefanywa mwalimu kusomesha mambo manne kwenye ile ile skuli aliyosoma. (page 194)
“Idadi ya wanafunzi imezidi kwenye klasi kutoka ishrini na tano kufika mpaka wanafunzi thamanini.” (page 195)
Serekali ya makomred imeleta walimu kutoka Urusi na Jarmani ya Mashariki. Wengi wao walikua hawajui Kingereza vizuri. Wanafunzi hawafahamu kitu kwao. (page 195).
Makomred ni majoga na mabarakala (Opportunists)“I cannot compromise with opportunism, for he who compromises with opportunism is bound to be an opportunist himself.”              Ali Sultan Issa (page 75)
Kwanza tumsikilize Komred anasema nini juu ya wale madhlumu walio nyang’anywa mali yao na wakafukuzwa majumbani mwao: “Wale waliobakia hawakuweza kufanya chochote. Imewabidi wasalim-amri, au tulijua wapi pakuwapeleka. Hawakuweza kusema ‘nyo’. Wote walikua majoga, na hatukupata upinzani wa kunyang’anya. Nani atathubutu?”, (page 101).
Sasa tumsikilize anasemaje juu ya makomred? “Kwa miaka yote baada ya mapinduzi, ilitubidi tukae na hadhari; ilibidi tuangalie tunakwenda wapi, tunaonana na nani, na tunasema nini. Ilibidi tufikiri kabla hatujasema. Tukijua watu wanapotea; hapana asiejua kwamba watu wa dasturi wakituhumiwa kutaka kupinduwa serekali na wakiuwawa. Watu wakipotea na hawaonekani tena.Kila siku zikipita mambo yakizidi kuharibika.
Kwa hakika, mtu akiwa mwenye itikadi basi maisha zama za Karume yalikua mazuri sana.” (page 127).
Mistari ya watu kujipanga kununua chakula ilijaa nchini. Shetani anasimulia: “Siku moja tukiendesha gari (pamoja na mkewe wa Kizungu) tukaona watu wamejipanga mstari, na ijapokuwa tulikua sisi wawili tu ndani ya gari, nimemuambia: Ssshhh! Mzee atasikia!” (page 128).
Komred anasema: “Hatukutaka kumkosoa Karume- kwani yeye alikua ndie bwana mkubwa” (page 129).
Makomred na Wazee Wao
Tukuimchukulia Komred Ali Sultan kwakua ni kiongozi wa mbele kabisa wa makomred, tutapata kujua watu hawa vipi.
Mama yake: Tumekwisha ona huko mbele alipomsifu mama yake kua ni malaya. Akilipwa pesa na wanaume wake.
Baba yake: Pia huko mwanzo tumeona heshima yake kwa baba yake alipo ombwa na wazee wa chama cha ZNP kumtaka radhi baba yake, akakataa. Na akamtaka baba yake amshike yeye miguu na amuombe radhi.
Ami yake: Huyu ami yake ameuliwa Mfenesini, Unguja siku za mapinduzi. Komred Ali Shetani anatoa sababu ya kuuliwa huyu shahid: “Lazima aliishi vibaya na watu wa jirani yake”, (page 88)
Mkwe wake: Huyu ni shahid mwengine alie uliwa kwa dhulma ya bure. Lakini bora atusimlie Komred wetu hadithi yake: “Mkwe wangu, Amour Zahor, ameuliwa pamoja na kikundi cha watu walio tuhumiwa kuwa ni maadui wa mapinduzi. Watuhumiwa hawa hawakupelekwa kortini. Nimesikia yeye na wenziwe wamechukuliwa tu pahali na wakapigwa risasi. Risasi haikumuuwa, kwa hivyo mkwe wangu akaomba amalizwe. Badili yake, wauwaji wake wamemfukia nae bado yuhai pamoja na wenziwe. Alikua kibaraka, kwa hivyo kuuliwa kwake hakunishitua au kunipunguza kasi”, (page 100-101)
Makomred si Wafrika na wanadharau WaafrikaBaada ya kuuliwa Karume, Shetani hakujua bado nani wala nini limetokea. Akamuambia mwenziwe: “Ikiwa mmoja katika makomred kafanya kitendo hichi, basi tumo mashakani, na sote tutakufa. Hasa ikiwa wamempiga Karume, na Karume hajafa, sote tutauliwa. Lakini ikiwa Waafrika wamefanya haya wenyewe kwa wenyewe, basi tutakuwa hatuna matata.”, (page 133).
Anafakhari na mwanawe wakiume akisoma Uengerza kuwa “kapigana na mtoto wa kiume aliemwita ‘Muafrika’ ”, (page 146).
“Pia kutengenza na kuhifadhi miundombinu haijapata kuwashughulisha watu wajinga waliotoka misituni”, (page 128)
Makomred wamemuuwa KarumeMakomred wameshirikiana na Karume kwa kila hatua alizo zifanya tokea mwezi 12 Januari 1964 mpaka mwezi wa Februari 1972. Kheri, na shari wao wamebeba dhambi pamoja nae. Kuuwa, kufunga watu, kuharibu uchumi, afiya, ilimu, adabu na hishma. Kunyang’anya mali watu, kupiga watu viboko, kuwagawa watu na kupiga vita kabila mbali mbali, Warabu, Wahindi, Wangazija, Magoa, Mabahrani na hata Washirazi pia.
Karume na Nyerere walipowafukuza makomred hapo mwezi wa Februari 1972, ndipo Babu na wafuasi wake wakafanya mpango wa kumuuwa Karume mwezi 7 April 1972, baada ya kufukuzwa kwa mwezi mmoja na nusu tu. Halafu wakamsingizia Humoud Mohamed Barwani kuwa yeye kafanya kitendo hicho ili kulipiza kisasi cha baba yake. Sikweli. Ali Sultan anatuambia kuwa Babu amefanya mpango kumuuwa Karume, akafika mpaka ufukoni wa Unguja, halafu akarudi Dar-es-Salaam, bila ya sababu inayojulikana. Hapo wafuasi wake Zanzibar wakakata shauri ya kuendelea na mpango wao wa kumuuwa Karume. (page 136-137)
Anasema nini?
Ali Sultan anatuambia kua “mapinduzi hayakuwa mauwaji ya halaiki (genocide)”, (page 86), halafu anatuambia kwamba “kiasi ya theluthi ya Warabu wa Unguja wameuliwa au wamefukuzwa nchi.” (page 87).
Anasema: “Ninaweza kusema Seif Bakari alikuwa gozi mbaguzi, kwa sibabu hajapata kuowa mwanamke wa Kiarabu. Ambao ndio ulikuwa mtindo wa siku zile”, (page 126)
Anatuambia: “Ilinibidi kuweka benki (pesa za kigeni) na nizigeuze shilingi za Tanzania. Ambapo wageni hapa wakipata wanawake wetu wote kwa sibabu wanazo dola. Nchi gani hii? Ilikuwa ni upumbavu kuishi kwenye hali kama hii. Hiyo ilikuwa ni sababu moja ya mimi kutaka kupigania mabadiliko ya katiba.”, (page 150)
Baada ya kutoka jela mwaka 1979 kenda Uengereza akakutana na makomred wenziwe. Wakazungumza haja ya katiba mpya. Anasema: “Tunataka demokrasia na kusitisha hukumu kwa dikrii. Tunataka kufungua biashara ili watu wapate vitu waweze kuishi. Serekali lazima iachie uchumi mchanganyiko…. Kwani hata Uchina ina uchumi wa mchanganyiko hivi sasa” (page 151). Halafu Komred anatuambia: “Ni makosa ya Marekani, wliotujaza vichwani mwetu fikra za soko huru, ubepari na demokrasia” (page 166).
Komred Shetani anasema: “Kwa hakika, Seif Bakari na watu wa Youth League ndio takriban sababu ya maovu yote yalio tokea baada ya mapinduzi”, (page 126). Huyu Komred anatuambia nini hapa? Alikuwa wapi yeye na makomred wenziwe tokea siku ya mapinduzi mpake wiki sita kabla ya kuuliwa Karume? Huyu Komred pamoja na makomred wenziwe wameshirikiana na mapinduzi kwa muda wa zaidi ya miaka minane, halafu anamsingizia Seif Bakari. Je! Alikua amekwisha vuta bangi yake aliposema haya?

No comments:

Post a Comment