Tuesday, April 26, 2011

JE JOHN OKELLO NI SHUJAA ALIYEWAKOMBOWA WAZANZIBAR AU NI MARCENARY ALIYELETWA KUWAUWA WAZANZIBAR?

 
    JANUARI 12 ni siku ya kukumbuka Mapinduzi ya Zanzibar yapata miaka 44 iliyopita. Lakini jambo moja ambalo katika historia ya mapinduzi hayo ni kukosekana kwa mtu muhimu aliyeyashiriki.
    Jambo hili linaweza kuwa na mwangwi wa kibaguzi au wa kuwatenga katika kumbukumbu za tukio hilo muhimu lililoondoa utumwa na utwana uliokubuhu visiwani Unguja na Pemba. Mtu huyo ni Field Marshal John Okello.
    Mapinduzi
    Kumbukumbu za historia zinaonyesha kuwa Okello aliingia Zanzibar mwaka 1963 na kuwasiliana na viongozi wa Umoja wa Vijana wa Chama cha Afro-Shirazi (ASP). Kundi hilo lilikuwa linajipanga kuangalia namna ya kuondoa utawala wa Waarabu.
    Akiwa Zanzibar, Okello alikuwa mwanachama wa chama cha wapiga rangi – akiwa anapaka rangi majumba mbalimbali. Wakati wa muda wake wa ziada alikuwa akiunda kikundi kidogo cha askari wa Kiafrika.
    Kikundi hiki cha kijeshi kilishika na kufuata amri zilizokuwa zinatolewa Okello kama kiongozi ambazo ni pamoja na kutojihusisha na masuala ya ngono, kutokula nyama mbichi na kutokunywa pombe.
    Inaelezwa kuwa Okello alikuwa muumini mzuri wa dini. Aliamini kuwa alipewa amri hizo na Mungu akiwa kwenye ndoto kuuondoa utawala wa mabavu wa Waarabu na kuanzisha serikali ya mapinduzi ya Zanzibar na Pemba.
    Usiku mmoja kabla ya mapinduzi hayo, Okello aliwaamuru watu wake kuua vijana wote wa Kiarabu waliokuwa na umri kati ya miaka 18 na 25, lakini wasiwadhuru kina mama wajawazito na wazee na pia wasifanye ubakaji.
    Uasi
    Januari 12, 1964 akiwa anaungwa mkono na asilimia kubwa ya watu waliokuwa wanakandamizwa – wengi wao wakiwa Waafrika – Okello na kikosi chake waliweza kuingia katika mji wa Stone Town, Zanzibar, kulikokuwa maskani ya Sultan.
    Inaelezwa kuwa takriban watu 10,000 waliuawa, licha ya kwamba kikosi cha Okello kilikuwa na silaha duni. Okello na kikosi chake walilishangaza Jeshi la Polisi Zanzibar na kuchukua ofisi zao.
    Kwenye hotuba yake iliyotangazwa kwa njia ya redio, Okello alitangaza kuwa yeye ni ‘Field Marshal wa Zanzibar na Pemba’ na alimwamuru Sultan aue familia yake na kisha ajiue mwenyewe, la sivyo Okello ataifanya kazi hiyo mwenyewe.
    Hata hivyo, Sultani mwenyewe alikuwa tayari ameshajipatia maficho ya usalama nchini Uingereza, na waziri mkuu pamoja na mawaziri wengine pia waliwahi kutoroka.
    Kuwekwa pembezoni
    Kutokana na kufanikiwa kwa mapinduzi hayo, Okello alitangaza Baraza la Mapinduzi na Sheikh Abeid Amani Karume kuwa Rais. Kiongozi wa Chama cha Umma, Abdulrahman Mohamed Babu, akawa waziri mkuu. Baadaye alikuja kuwa Makamu wa Rais.
    Sheikh Karume na Babu hawakuwa wamejulishwa kuhusu mapinduzi hayo ya kijeshi kwani wote walikuwa Tanganyika, lakini walirudi Zanzibar walikokaribishwa na Okello.
    Lakini pamoja na shughuli yote aliyoifanya si Karume wala Babu waliomhitaji tena. Okello aliondoka kuelekea Tanganyika na kuanzia wakati huo alizuiwa kurudi Zanzibar na alipigwa marufuku pia asionekane Tanganyika na Kenya.
    Utata kuhusu kifo chake
    Baada ya Okello kupigwa marufuku Zanzibar na Tanganyika, aliishi maisha ya kuhamahama kutoka nchi moja hadi nyingine. Aliishi Kenya na baadaye Congo Kinshasa na Uganda. Aliwahi kufungwa mara kadhaa na mara ya mwisho alionekana akiwa na kiongozi wa Uganda mwaka 1971 na baadaye alipotea.
    Katika kitabu cha ‘Revolution on Zanzibar’ kilichoandikwa na Don Petterson inadhaniwa kuwa Idi Amin alimwona Okello kuwa ni tishio kwake na mara nyingine inaelezwa kuwa baada ya Amin kujipandisha cheo na kuwa Filed Marshal, inaelezwa kuwa Okello alisema kwa dhihaka, “Uganda hivi sasa ina Field Marshal wawili.
    Hata hivyo inaelezwa kuwa Idd Amini alipanga mipango ya mauaji dhidi ya Okello, lakini pamoja na hali hiyo kifo chake kimebakia kuwa ni cha utata.
    Alikotoka
    John Gideon Okello alizaliwa mwaka 1937 wilayani Lango, Uganda. Ni mwanamapinduzi asiye na kifani barani Afrika.
    Lakini licha ya kuongoza Mapinduzi ya Zanzibar mwaka 1964 yaliyouondoa utawala wa Sultan Jamshid bin Abdullah na kuwezesha kuanzishwa kwa Jamhuri ya Zanzibar, pia amekuwa hafahamiki sana.
    Alianza kuishi maisha ya uyatima akiwa na miaka 11. Alipofikisha umri wa miaka 15 aliondoka nyumbani kwao na kwenda kutafuta ajira katika maeneo mbalimbali ya Afrika Mashariki.
    Kuanzia mwaka 1944 alikuwa amefanya kazi nyingi ikiwa ni pamoja na ukarani, mtunza bustani na mfanyakazi katika idara na shughuli mbalimbali. Hata hivyo, alijifunza kufanya biashara ya kuuza matofali na baadaye alimudu kufanya kazi ya uashi, lakini alikamatwa mjini Nairobi, kutokana na sababu ambazo hazikuelezwa; hata hivyo yeye mwenyewe aliwahi kuelezwa kuwa alikamatwa kutokana na makosa yaliyohusiana na hali ya jinsia. Alifungwa miaka miwili gerezani. Kifungoni ndiko kulikomfanya awe na fikra za kimapindizi.
    Mara nyingi umekuwapo uvumi kuwa huenda Okello alikuwa amepata mafunzo yake nchini Cuba, lakini jambo hili halikuwahi kuthibitishwa na Okello mwenyewe.
    Mwaka 1959 aliingia kisiwani Pemba katika harakati zake za kutafuta ajira kwenye mashamba ya karafuu, lakini badala yake alijiunga na jeshi la polisi.
    Hata hivyo, baadaye alijiunga na Chama cha Afro-Shirazi kilichokuwa kinapinga jamii ya watu wachache kuhodhi uchumi wa Zanzibar na Pemba.
    Kuna wengi walifanya mambo yanayofanana na Okello. Miongoni mwao ni Ernesto Guevara de la Serna maarufu kama Che Guevara, aliyeshiriki kikamilifu kwenye mapinduzi ya Cuba licha ya kwamba alikuwa ni mzaliwa wa Argentina.
    Leo hii Che Guevara ni jina linalosifika na kuheshimika nchini Cuba kutokana na mchango wake. Haiyumkiniki jina la Okello nalo lingekuwa ni jina la kuheshimika kwenye na kukumbukwa kwenye Mapinduzi ya Zanzibar lakini ndivyo imekuwa sivyo.

    No comments:

    Post a Comment