Sunday, August 14, 2011

DR SHEIN AJARIBU KUFUNGUWA UCHUMI WA ZANZIBAR

 
UONGOZI wa Wizara ya Biashara,Viwanda na Masoko umetoa pongezi kwa Viongozi Wakuu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kuchukua hatua mbali mbali za kuthibiti na kuendeleza zao la karafuu.
Uongozi huo ulieleza hayo leo huko Ikulu mjini Zanzibar katika kikao kilichoongozwa na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk. Ali Mohamed Shein,cha kukutana na viongozi wa Wizara za Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kwa kuangalia mipango ya utekelezaji wa malengo makuu ya Wizara na uhusiano wake na Dira 2020 na MKUZA pamoja na mpango kazi wa kufikia malengo hayo.
Katika kikao hicho maalum Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, maalim Seif Sharif Hamad na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd walihudhuria.Wizara hiyo ya Biashara ilieleza mipango yake na mikakati iliyojiwekea katika robo ya kwanza ya mwaka wa fedha 2011/2012 ambapo pamoja na mambo mengineyo ilitoa pongezi kwa viongozi Wakuu kutokana na ushiriki wao kikamilifu katika uhamasishaji wa uvunaji na kule kuwataka wananachi kuuza karafuu zao katika Shirika la ZSTC.Uongozi huo ulieleza kuwa miongoni mwa mikakati ya kuliimarisha zao hilo pamoja na kuwapa tija kubwa wananchi nchi ni kule kuunda Kikosi Maalumu cha kuratibu uchumaji na uuzaji wa zao la karafuu kilichozinduliwa hivi karibuni na Rais Dk. Shein huko Pemba.Aidha, uongozi huo ulieleza jitihada zake ulizochukua katika kuweka msingi wa kisera wa ununuzi wa zao la karafuu kwa wakulima ambapo sasa watalipwa asilimia 80 ya bei ya soko la dunia.Pamoja na hayo, uongozi huo ulileza kuwa juhudi nyengineyo iliyochukuliwa ni kurekebisha bei ya karafuu kutoka wastani wa Tshs. 5000 hadi Tshs. 1000 kwa kilo moja ambapo kwa msingi huo wa kisera serikali imeendelea kurekebisha bei kwa wakulima na sasa bei hiyo ni Tshs 15,000 kwa kilo moja sawa sawa na Tshs.22,000 kwa pishi.Wizara hiyo ilieleza mikakati yake iliyojiwekea na ile ambayo imeshaanza kutekelezwa ambapo katika kupambana na hali ya mwenendo wa jumla wa bei kwa bidhaa muhimu hasa chakula, serikali ilichukua hatua za kisoko ambazo zilizihusisha kufanya mashauriano na wafanyabiashara, kuandaa kanuni mpya na taratibu za ufanyaji biashara, usimamizi na ukaguzi wake.Ilieleza kuwa chini ya utaratibu huu mpya bei za bidhaa hasa chakula sasa zinapangwa kwa kushirikiana baina ya Serikali na wafanyabiashara wenyewe.Wizara ilieleza kuwa kwa ujumla, utaratibu huu umejitokeza kufanyakazi vizuri ambapo bei za chakula ukiwemo mchele, unga wangano na sukari zimekuwa na mwenendo wa utulivu kwa sasa.Aidha, Wizara hivi sasa inaandaa utaratibu wa kujumuisha bidhaa nyengine muhimu kama vile mafuta ya kupikia, vifaa vya ujenzi hasa saruji na mabati katika mfumo huo.Uongozi huo ulieleza kuwa kwa madhumuni ya kuhuisha sekta ya viwanda na kwa lengo la kuitayarisha Zanzibar vizuri kuwa mshiriki thabiti katika biashara na uchumi wa kikanda, Serikali imeanzisha juhudi mpya za kuiwezesha Zanzibar kuwa mshiriki imara katika mfumo wa Soko la Pamoja la Afrika Mashariki na lile la SADC.Pamoja na mambo mengineyo, uongozi huo wa Wizara ya Biashara, Viwanda na Masoko ulieleza hatua na malengo yake ya kumlinda mtumiaji, kuimarisha mazingira bora ya ukuzaji biashara na kuimarisha mazingira ya uwekezaji katika sekta ya viwanda.Pia, Wizara ilisisitiza haja ya kuongezwa uzalishaji wa mazao ya chakula hapa Zanzibar ambapo pia, Dk. Shein alisisitiza haja ya kuliimarisha zao la nazi kutokana na umuhimu wake mkubwa na kueleza kusikitishwa kwake na hali ya ukataji wa minazi ovyo.Viongozi wote wakuu walioshiriki chini ya Mwenyekiti wa kikao hicho Rais Dk. Shein, walipongeza juhudi zilizoanza kuchukuliwa na Wizara hiyo.Wakati huo huo Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein kesho anatarajiwa kuanza ziara ya siku tatu kisiwani Pemba ambapo mbali na mambo mengineyo ataangalia Kituo cha ununuzi wa Karafuu (ZSTC) kilichopo Daya Mtambwe na kile cha Mkanyageni pamoja na kuangalia kambi za karafuu.
Aidha, atatembelea Kituo cha Ununuzi wa Karafuu (ZSTC) Chake Chake, kukagua Kambi ya Karafuu Mahudusi ya, Mtuhaliwa, kuangalia ununuzi wa karafuu katika kituo cha ununuzi wa karafuu Mkanyageni na kukagua kambi za karafuu Changaweni.Sambamba na hayo, Dk. Shein atakagua kituo cha ununuzi wa karafuu Mkoani ZSTC ambapo pia ataungana na wananchi wa Mikoa yote miwili ya Pemba katika futari aliyoiandaa kwa siku tofauti atakazokuweko kisiwani humo.

No comments:

Post a Comment