Monday, August 22, 2011

NIA YAO NI KUVUNJA UISLAM ZANZIBAR KIWE KISIWA CHA KUFANYA ULANISI KAMA VISIWA VINGINEVYO ULIMWENGUNI


 
Nianze kwa kuangalia historia ya Zanzibar huko nyuma kidogo kabla ya Mapinduzi yanayojulikana kama matukufu kwa baadhi ya waumini wa Mapinduzi hayo, huku baadhi ya walio wengi hadi leo wanaamini kwamba Mapinduzi hayo yalikuwa ni janga kuu ambalo liliikumba dola ya Zanzibar.Historia inatufunza mengi juu ya Mapinduzi yaliofanywa kuipundua dola huru ya Zanzibar lakini pia kwa Wazanzibar kupoteza utaifa wao kwenye ramani ya ulimwengu ni suala la kujadiliwa kwa undani kabisa.
Ni dhahiri kwamba Historia ya Zanzibar imepotoshwa na baadhi ya Wahafidhina wachache ili kulinda maslahi yao na pia kuendeleza ile siri nzito ambayo walio wengi hususani vizazi vipya vimeshindwa kuelewa historia ya Visiwa hivi mashuhuri katika mwambao wa Afrika Mashariki.Ni huzuni lioje kwa Wazanzibar leo hii, ambapo kwa sasa wengi wao wamesambaratika na kuviacha visiwa vyao kama vile hawavijui au hawakuzaliwa ama kuishi humo katika maisha yao.
Uislam Zanzibar ndio uliokuwa dira na mfumo wa maisha wa mabibi na mababu zetu,hili lilikuwa wazi na kila Mzanzibar wakati huo aliheshimu na kufuata mila na silka za utamaduni huo.
Zanzibar ilisifika kwa mfumo mzuri wa elimu ya dini na kwa vile Wazanzibar walijitokeza kuonesha umahiri wao katika fani hiyo, jambo ambalo iliifanya Zanzibar kuonekana kama ni lulu na kitovu cha Uislam katika mwambao wa Afrika Mashariki na kati, wakiongoza kwa Mamufti na Maimamu wakubwa wenye elimu, vipaji  na hadhina marudufu ya dini ya kiislam.
.
Wakati huo huo historia pia ilituonesha ni jinsi gani Mataifa makubwa kama vile Mwengereza na Roma walivyokuwa wakifanya kila lilowezekana kuona kwamba ukristo unazagaa na kuabudiwa Duniani, huku wakipanga mbinu za kuzitawala baadhi ya nchi ambazo walihisi zilikuwa na maslahi makubwa ya kiuchumi kwao.Pia Wakoloni hawa waliitumia dini ya kristo kama ni silaha ya maridadi ya kuzitawala zile nchi ambazo kwa upande wao zilikuwa na maslahi nazo, kwa maana hiyo Uislam ilikuwa ni kikwazo kwao na ulitishia maslah kwao, na haikuwa rahisi kwao kujipenyeza bila kutumia mbinu hii ya dini na uokozi.Mwingereza aliingia ukanda wa Afrika mashariki kwa mtindo wa kusambaza dini, jambo ambalo halikuwa kikwazo kwa kuikamata Tanganyika licha ya kwamba Tanganyika Uislam ulikuwa mkubwa kabla ya kuja kwa Wakoloni hao wa Kijeruman na Waingereza.
Mwengereza alicheza karata mzuri dhidi ya Tanganyika na kuwabatiza walio wengi kwa maana hiyo hakuwa na kazi kubwa kuwasambaratisha Waislam kule Tanganyika. Hii iliwezekena kirahisi tu pale Watanganyika walipoanza kudai uhuru wao na kuona njia pekee kwa wao kupata uhuru kwa urahisi ni kumchagua kiongozi ambae ni mkiristo ili iwe rahisi kwa wao kukubalika na Mataifa makubwa na kujikomboa.Mwalimu Nyerere alionekana ndio mtu pekee kwa wakati ule na hapa Mwengereza hakusita kuitumia nafasi hiyo kumpika Mwalim Nyerere na kumuahidi kumlinda ili kuutetea Ukristo kwa Maslahi ya Mwengereza na Waroma.
Baada ya kufanikiwa agenda yao hiyo na kuiuwa ile East africa muslim agency, Mwalim Nyerere alipewa jukumu la kuidhibiti Zanzibar jukumu ambalo halikuwa rahisi kwa wakati huo. Jukumu hili lihitaji maarifa,mali, mipango,agenda na akili ya hali ya juu, kwani kinyume chake ingeleta tatizo sio kwa Afrika Mashariki tu lakini hata Duniani kwa zile nchi zenye uislam na itikadi pamoja na msimamo mkali wakati huo.Mbinu na msaada  mkubwa ulihitajika ili kuona kwamba Wazanzibar wanashindwa kung’amua mbinu hizo za Wakoloni hao ambazo alikabidhiwa Mwalim Nyerere kuuwa Uislam Zanzibar.
Shauri hili liliwauma vichwa sana Waingereza hatimae wakaamua kuandaa mpango wa siri zidi ya Zanzibar kwa kumtumia Mwalim Nyerere kuandaa mpango wa kuidhibiti Zanzibar.
Shauri ambalo alishauriwa Mwalim Nyerere ni kufanya Muungano kwa kisingizio cha kuisadia Zanzibar katika mambo ya kiulinzi. Lakini katika agenda hiyo Nyerere alisisitizwa kwamba lazima awe muangalifu na afuate masharti yote kwani kutozingatia masharti hayo ni kuwashtua Wazanzibar ambao kwa wakati ule macho yao yalikuwa wazi kung’amua hila na  mbinu hizo.
Moja ya sharti alilopewa Mwalim Nyerere ni kwamba mpango ulioandaliwa ni wa muda mrefu kwa maana hiyo hautakiwi kufanyiwa haraka, kwa vile Zanzibar imashekubali kuungana nao japo kwa hila na mbinu, hali lazima iendelee hatua kwa hatua mpaka Wazanzibar wasalimu amri wenyewe.
Waingereza walimwambia Mwalim Nyerere kwamba mpango wao utakuchukua nusu karne au ikibidi karne mzima kufanikiwa kwani sio jambo rahisi kukubalika kwa Wazanzibar ambapo kwa wakati huo asilimia ya Waislam ilikuwa mia fil mia.Walibuni mbinu nyingi lakini moja wapo ni kuona inapofika nusu karne tokea Mapinduzi  kuasisiwa na kuunganishwa kwa Zanzibar na Tanganyika lile wimbi la uislam kiimani liwe limeondoka na iwe  adhana inashindikana kusikilizwa Zanzibar. Lakini katika kipindi hichi cha mpito Wakristo wazidi kujiimarisha na kujipenyeza Visiwani huku wakiimarisha Nyumba za ibada yaani Makanisa kila kichochoro. Mbinu hii ifanywe kwa umakini mkubwa bila ya wenyewe kushtuka ili wakija wakiamka waone tayari Zanzibar imekuwa na mchanganyiko mkubwa  kati ya waumini wa Kiislam na Wakristo, jambo ambalo leo hii wamefanikiwa sana Visiwani.
Mwalim Nyerere alipewa draft mzima wa mpango huu na aliutumia kwa makini na usiri mkubwa sana, ndio maana ukaona kila mwaka katika sherehe za Muungano Mwalim Nyerere kwa kutumia Serikali yake Tanganyika alikuwa akiimega Zanzibar kwa kuchukua baadhi ya viungo muhimu vya Serikali ya Zanzibar na kuviingiza kwa ujanja kwenye Muungano huku maskini Wazanzibar wakishindwa kuelewa siri iliopo hadi leo hii tayari Zanzibar imeshatoweka.
Tanganyika ilianza kuimegua Zanzibar kupitia vyombo vya dola,fedha, na pia utaifa kwa kuondosha maksudi hatia ya kusafiria ili Watanganyika waingie Zanzibar kwa urahisi ili wauimarishe ukristo na kuupunguza nguvu uislam jambo ambalo wamefanikiwa kwa kiasi kikubwa. Historia inaonesha kwamba kabla ya Muungano wa Zanzibar na Tanganyika, Zanzibar kulikuwa na makanisa machache ambayo yanajulikana na hata waumini wake idadi yao pia ikifahamika lakini leo hii ni tofauti, karibuni uwiano utakuwa sawa kati ya waislamu na wakristo.
Pia idadi ya baa zimeongezeka,ukahaba pia umechukua nafasi yake lengo ni kuona kwamba Wazanzibar wanaacha mila , desturi , silka na utamaduni wao matokeo yao wanajichanganya na kusahau maadili yao.Na hili limekuwa likiendeshwa kwa siri kubwa huku Serikali ya Muungano ikilibeba bango hili bila Wazanzibar kujielewa ni kitu gani kinaendelea. Wazanzibar hawana budi kuielewa mbinu hii, kwamba ni mpango maalum ulioandaliwa kwa muda mrefu na umefanikiwa sana, tuitazeme Zanzibar leo iko wapi ? Pia vibaraka wa Zanzibar wanapewa asali ili waimung’unye kwa maslahi madogo tu ya vyeo, kumbe maskini ndio hivyo wanaimaliza Zanzibar na watu wake, huku wao wakivalishwa rubega shingoni.

No comments:

Post a Comment