Sunday, February 24, 2013

ROBERT MUGABE-CCM KITU KIMOJA-ATAKA KUGOMBEA TENA URAISI



RAIS wa Zimbabwe Robert Mugabe  ametangaza kushiriki kwa mara ya sita kwenye uchaguzi wa urais utakaofanyika nchini humo.
Mugabe alisema hayo wakati  wa sherehe ya  kuadhimisha siku yake ya kuzaliwa kwake ambapo alitimiza miaka 89.
Katika hafla hiyo kiongozi huyo alisema kuwa, kumekuwa na hila pamoja na shinikizo mbalimbali kutoka Marekani na Uingereza kwa lengo la kumwondoa madarakani yeye pamoja na chama chake cha Zanu PF.
Mugabe ambaye anaiongoza nchi hiyo kwa zaidi ya miaka 33 sasa amepanga kufanya sherehe kubwa zaidi ya kuzaliwa kwake mwezi ujao itakayogharimu kiasi cha Dola 600,000.
Wakati Rais Mugabe akijiandaa kufanya sherehe mwezi ujao, Waziri wa Fedha wa nchi hiyo Tendai Biti alitangaza kuwa, nchi hiyo imebakiwa na hazina ya Dola 300 kwenye Serikali ya nchi hiyo.
Zimbabwe licha ya kukabiliwa na hali ngumu ya kiuchumi na vikwazo vilivyowekwa na nchi za Magharibi, inatuhumiwa kwa hali mbaya ya ukiukwaji wa haki za binadamu.
Awamu ya tano ya uchaguzi wa Rais nchini humo uligubikwa na ghasia pamoja na vurugu  zilizosababisha Chama cha Zanu PF na kile cha MDC kinachoongozwa na Morgan Tsvangirai kuunda Serikali ya umoja wa kitaifa nchini humo.
Mwanzoni mwa mwezi huu Waziri wa Masuala ya Kikatiba Eric Matinenga alisema  kura  ya uamuzi kuhusu Katiba Mpya itafanyika mwezi Machi.
Serikali hiyo ambayo imefilisika imeomba Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) kuisaidia kupata Sh21.48 bilioni kuendesha kura hiyo pamoja na uchaguzi.
“Nilipata ujumbe kutoka kwa Ofisi ya Rais kwamba tarehe ya kura ya uamuzi tayari imeafikiwa. Kura hiyo itafanyika Machi 16,” Matinenga aliwaambia wanahabari mjini Harare.
Katiba ya sasa ya taifa hilo la Kusini mwa Afrika, ambayo imefanyiwa marekebisho mara 19, ilianza kutumika baada ya Zimbabwe kujipatia uhuru kutoka kwa Uingereza mnamo 1980.

No comments:

Post a Comment