Tuesday, July 7, 2015

ALLY SALEH-HAKUWEZI KUWA NA UCHAGUZI WA HAKI ZANZINAR

Screenshot_2015-07-07-20-26-07-1
Ally Saleh
1 July at 07:56 ·
Makala yangu niloandika katika gazeti la Mtanzania la leo Jumatano ya Julai 1, 2015
HAKUWEZI KUWA NA UCHAGUZI WA HAKI ZANZIBAR
NA ALLY SALEH
Tunaandika na tunasema, tutasema na tutaandika kwa ajili ya kuwepo rekodi kesho na kesho kutwa kuwa kulikuwa na watu waliandika na kusema. Sababu ya kuweka rekodi ni kuwa huko mbele ya safari itakuja kusemwa mbona hawakusema, kwa hivyo tunaandika ili rekodi ije iseme. Rekodi itakuja kusema kuwa kuna watu toka mwanzo kabisa wamesema kuwa kwa hali inavyokwenda hakuwezi kuwa na uchaguzi huru na haki mwaka huu. Hakuwezi kabisa kwa sababu kila dalili zinaonyesha hivyo wazi na dhahir shahir. Tunaandika ili tuache kudanganyana kuwa yanayotokea sasa ni matokeo ya kawaida na kuwa yakiwachiwa yatapoa tu na yatasahauliwa ilhali tunajua kuwa dosaari ya kitu huanza mwanzo kama tusemavyo dalili ya mvua ni mawingu. Na hivi sasa si mawingu tu bali hata mvua imenyesha labda sasa tusubiri kimbunga na gharika.
Na tuondoe shaka kwa mambo tulivyoanza kuyaona ni hakika kuwa kimbunga na gharika kinakuja nacho ni kule kutokea fujo za uchaguzi kuanzia wakati huu mpaka wakati wa kutangazwa matokeo ya uchaguzi baada ya kupigwa kura Oktoba 25. Nimeanza kupoteza imani na kwa hakika kuingiwa na hofu kuwa kuna watu na makundi ya watu ambao wanatengeneza mazingira ya kuufanya Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu usiwe kabisa huru na haki na nasema mapema kuwa tusijidanganye kuwa tutakwenda na kumaliza salama. Si kweli na thumma si kweli. Haiwezekani zoezi la uendeshaji la wapiga kura liendeshwe kihuni, kibabe, kikora, kimwamba kama inavofanywa hivi sasa na kisha tuwe na uchaguzi huru na haki, wakati uhuru huo umeshaanza kupondwa pondwa na haki hiyo imeshaanza kunyakuliwa. 
Inakuwaje matendo yanayofanyika wakati huu wa kuandikisha wapiga kura, kwa uroho wa watu na makundi ya watu kufanya matendo akhasi ya matendo, vitisho kupita vitisho, wizi na hadaa kupita mipaka kisha tukae tuseme kuwa ifikapo Oktoba kutakuwa na uchaguzi wa huru na haki. Ni kujidanganya. Mimi sitaki niwe katika ambao watakuwa na moyo wa kujidanganya wakati makundi ya vijana yakiwa na silaha, yakijiziba nyuso na huku bila sare rasmi za Polisi, Jeshi wala Vikosi vya Zanzibar yakifanya vitendo visivyokubalika kidemokrasia na huku mamlaka zikinyamaza kimya halafu tuseme tutakuwa na uchaguzi huru na haki. Wao wakifanya hivyo wakikiuka taratibu zote za kikatiba na kisheria kwa ajili ya kujaliza mapandikizi kwa njia za nguvu katika Daftari la Kuduma la Wapiga Kura (DKWK) mamlaka zinyamaze kimya na kujidai hazijui wala hazioni vitendo hivyo, haiwezekani wala haikubaliki. Iwe anaepanda jukwaani kudai vitendo hivyo ni haramu na viovu ahojiwe na ashutumiwe kwa uchochezi ilhali mfanyaji wa matendo ya kutisha watu wanaotaka kupiga kura na kupeleka watu kwa nguvu katika vituo wasivyohusika hata haulizwi kitu kunanifanya niamini hapatakuwa na uchaguzi huru na haki.
Kijana mmoja anaedaiwa kuzuia watu wasiohusika na jimbo kujiandikisha kinyume na sheria asakwe kwa makundi yanayobeba magongo na misumeno na wakijitia masizi na Sheha kuhusika, ilhali wanaopeleka watu vituoni au kuwaleta mitaani na kuwapa vitambulisho vya Mzanzibari ili wawe wapige kura hawaulizwi kitu, kwangu si dalili ya kuwa tutakuwa na uchaguzi huru na haki na sitaki kudanganywa. Kuenea katika mtandao video ya vijana wakidaiwa kuwatusi viongozi kufanye vijana hao wakamatwe kama ni magaidi ilhali video nyengine zinaenea tena zikimhusu kiongozi ngazi ya Mjumbe wa Baraza la Wawakilishi akihamasiha katika kikao cha siri watu walio na asili ya Bara wajiandikishe kupiga kura kujaliza jimbo lake, na pakiwa na shaka na ukaazi wao kufikia kupata haki hiyo, kunanipa wasiwasi kuwa hatuwezi kuwa na uchaguzi huru na haki. Inapofika viongozi wa Polisi wanapohojiwa katika vyombo vya habari na kufanya ubabaifu wa kutojua kuwa kuna makundi hayo haramu, ambayo yanaranda wazi wazi na fawahisha na hata yakitumia magari ya Vikosi vya Zanzibar kunanipa nguvu kuwa sitodanganyiika kuwa kabisa kabisa hapataweza kuwa na uchaguzi huru na haki mwaka 2015.
Hivi sasa kukiwa na makundi makubwa ya vijana ambao wamekamatwa na Polisi kwa kufanya kazi ya kuzuia uharamia huo wa kupeleka watu vituo vya kuandikisha bila ya haki na sheria, pengine wakisubiri kufunguliwa mashtaka na wengine kupigwa na kuumizwa, ilhali hakuna hata katika makundi yanayovunja katiba na sheria aliekamatwa si ishara kuwa tutakuwa na uchaguzi huru na haki na sidangayiki kabisa. Sidanganyiki kuwa CUF walifanya nao walivyotaka huko Pemba na kwa hivyo hawana sababu ya kupiga kelele yanayofanywa au yaliofanywa Unguja. Sidanganyiki kwa maana CCM imesema mambo yameeenda uzuri Pemba na hatukusikia kabisa uharamia kiwango cha kijanawidi kilichotokea katika uandikishaji Unguja na Tume ya Uchaguzi ikiwa kimya kwa dhana kuwa yanayotokea nje ya vituo hawayajui. Najua yote haya, pamoja na madai ya kuandikwa watoto wadogo katika vitambulisho vya Mzanzibari ili wawe na haki ya kujiandikisha kupiga kura bila ya upinzani, si mambo ambayo yanakuzana uhusiano mzuri wa wananchi, wa kisiasa na mustkbali wao wa kuamua Serikali yao ijayo kwa njia ya haki, huru na salama.
Zikowapi taasisi za haki za binadamu Zanzibar na Tanzania, wako wapi Umoja wa Mataifa, Umoja wa Ulaya, Umoja wa Afrika na Jumuia ya Afrika Mashariki ili waione hali hii leo wakijua kuwa kila uchao itachafuka kuelekea Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 25. Dalili zote ziko wazi ingawa sivyo tuombavyo. Rais wa Zanzibar Dk Ali Muhammed Shein kumbuka utakuwa mas-uul namba moja ijapo yanayofanywa kwa sasa yanaweza kuonekana yatakuwa na maslahi nawe kwa minajil ya idadi ya kura. Kumbuka Zanzibar ilishaondoka huko, utakaeirudisha ni wewe, na umma wa Zanzibar utausha mzigo wote kwako, kama hukukemea na kuzuia leo.
Nakala ya Ali Saleh
KILA MZANZIBARI ATAULIZWA SIKU YA KIYAMA NA MWENYEZI MUNGU ULIPOSIKIA WAZANZIBARI WENZIO WANADHALILISHWA NA KULAWITIWA NA HAWA JE ULIFANYA NINI TAFUTA JIBU LAKO MAPEMA KWA SIKU HIYO YA KIYAMA SIKU AMBAYO MALI NA WATOTO WAKO WALA CHEO CHAKO HAVITAKUFAA SIKU HIYO.

No comments:

Post a Comment